ADAM Philip Kuambiana amezikwa jana kwenye
Makaburi ya Kinondoni jijini Dar es Salaam huku akiacha maswali magumu
matano kuhusu maisha, mazingira na hatimaye kifo chake, Risasi
Mchanganyiko linakupa moja kwa moja.
Marehemu Kuambiana alifariki dunia Jumamosi iliyopita asubuhi
akikimbizwa kwenye Hospitali ya Mama Ngoma, Mwenge jijini Dar es Salaam
kwa ajili ya matibabu baada ya kuugua tumbo ghafla.
Mwili wa marehemu Kuambiana ukiwasili kaburini tayari kwa shughuli za kuusitiri.
MANENO KUTOKA KWENYE MIDOMO YA WATU
Baada ya kifo chake, maneno kutoka kwenye vinywa vya watu yalionesha ni
maswali magumu ambayo majibu yake yangepatikana kama marehemu angekuwa
hai.
Hata hivyo, Risasi Mchanganyiko lilifanya kazi ya ziada kuhakikisha
maswali hayo yanapata majibu kwa ndugu au watu wa karibu na marehemu.
MASWALI MAGUMU MATANO
Maswali ya watu kuhusu marehemu Kuambiana yako matano ambayo baadhi ya
wasomaji walitoa ombi kwa Magazeti Pendwa ya Global kuyafanyia kazi na
kutoa majibu yake kwa vile uwezo huo kwa Global upo.
SWALI LA KWANZA
Inadaiwa kuwa asubuhi ya kifo chake, marehemu na wasanii wenzake
walikuwa kambini, Sinza jijini Dar. Wasanii hao walimgongea mlango kwa
sababu walitakiwa kwenda kurekodi filamu wakakuta mlango uko wazi,
wakaingia.
Je, ni kwa nini marehemu aliacha mlango wazi wakati kuna maelezo kwamba alikuwa akilala na vifaa vingine vya kufanyia kazi?
Stara Thomas ambaye amewahi kuwa mchumba wa marehemu, anajibu hili:
“Ninavyojua mimi Kuambiana alikuwa anavuta sana sigara. Mara nyingi
akitaka kuvuta alikuwa akitoka nje. Sasa huenda alfajiri ya siku hiyo
alifungua mlango akatoka kuvuta aliporudi hakuufunga tena.”
Adam Philip Kuambiana enzi za uhai wake.
SWALI LA PILI
Yapo madai kwamba, siku hiyo marehemu alikuwa na fedha nyingi. Hilo
linaweza kuthibitishwa na rafiki wa karibu wa marehemu ambaye alisema
kuwa, Ijumaa, yaani siku moja kabla ya kifo, Kuambiana alikuwa na fedha
nyingi.
Kuhalalisha hilo, hata mhasibu wa Gesti ya Silvarado, Sinza jijini
Dar ambayo marehemu na wasanii wake waliitumia kupiga kambi kwa ajili ya
kurekodia filamu alisema walikuwa wakimdai shilingi milioni mbili na
siku hiyo ya Ijumaa alilipa keshi.
Swali ni je! Kama marahemu alikuwa na fedha nyingi japokuwa
hakijajulikana kiasi, baada ya kifo chake zilichukuliwa na nani na
ameziweka wapi?
NDUGU WA MAREHEMU ANAJIBU
Ndugu wa marehemu ambaye alisema si msemaji wa familia na akaomba jina
lake lisitajwe, alisema anachojua yeye marehemu hakukutwa na hata senti
tano mfukoni.
“Hilo la kusema alikuwa na fedha siku hiyo hata sisi tunasikia tu.
Lakini sisi kama familia tunajua hakukutwa na pesa licha ya kwamba
tumesikia alikuwa akiwapa ofa watu kwenye mabaa. Kuna mtu nasikia
alitoweka nazo, tunamsaka kila kona.”
SWALI LA TATU
Wengi wanatatizwa na makazi ya marehemu kwamba mtu angetaka kumpata
Kuambiana angekwenda wapi maana mara nyingi alikuwa akionekana kwenye
baa mbalimbali za jijini Dar hasa maeneo ya Sinza.
“Mimi nimewahi kusikia kwamba, Kuambiana alikuwa hana makazi.
Alipokutana na Stara Thomas ndiyo akawa anaishi kwake, walipomwagana
ikawa mwendo ni uleule.
“Nimewahi kusikia kuwa alipokuwa akipewa tenda ya filamu ndiyo makazi
yake yalikuwa kambini. Lakini sina hakina sana makazi yake japokuwa na
mimi ni msanii wa filamu kama alivyokuwa yeye,” alisema mwigizaji mmoja
akiomba asindikwe gazetini.
STARA ATAJA MIKOCHENI
Risasi Mchanganyiko lilizungumza tena na Stara ambaye alijibu:
“Mimi aliniambia makazi yake yalikuwa Mikocheni (Dar) lakini sikuwahi kufika. Lakini ninavyojua ni Mikocheni.”
Akizungumza na gazeti hili msibani kwa mke wa marehemu, Bunju jijini
Dar, ndugu mmoja alisema anavyojua yeye marehemu alikuwa akiishi Bunju
B.
SWALI LA NNE
Baadhi ya mastaa walisikika wakisema baada ya kuachana na Stara,
marehemu alikuwa na uhusiano wa kimapenzi na msanii wa filamu anayeitwa
Lulu Jumanne ‘Selina’ Lakini swali likawa je, ni kweli?
mambo hadharan LAMSAKA, LAMPATA SELINA
“Ni kweli mimi na Kuambiana tulikuwa wapenzi. Baada ya kuachana na mke
wake wa ndoa (Janeth) alikuja kwangu tukaishi wote, lakini baadaye
tukaachana, nikasikia yuko na Stara.
“Hata hivyo walikorofishana na kurudi tena kwangu,” alisema Selina ambaye ndiye mpenzi wa marehemu hadi kifo chake.
SWALI LA TANO
Swali la tano ni kuhusu filamu aliyokuwa akiishuti marehemu ambayo
kaiacha katikati inayoitwa Jojo. Marehemu alisema ni yake lakini kuna
madai kwamba, Stara Thomas naye anadai ni ya kwake.
Risasi Mchanganyiko lilimsaka Stara juzi kuhusu madai hayo ambapo alisema:
“Mimi sina tatizo, kama marehemu alisema ni yake sawa tu. Ila ilikuwa
ya kwetu sote. Hata ikijulikana ni yake sidhani kama ni tatizo.”
AZIKWA
Marehemu Kuambiana alizikwa jana katika Makaburi ya Kinondoni, Dar
ikitanguliwa na misa iliyosomwa katika Viwanja vya Leaders Club,
Kinondoni ambapo aliagwa.
Mastaa kibao walifurika viwanjani hapo lakini wengi waliishiwa nguvu, kuanguka na kupoteza fahamu.